Ndugu wananchi wa Kalambo,
Muda wa kampeni umekwisha, sasa ni wakati wa kuungana,
kushirikiana na kushikamana katika kuijenga Kalambo yetu. Maendeleo hayaletwi
na mtu mmoja pekee, bali ni matokeo ya ushirikiano wa wananchi wote. Kila mmoja
wetu anapaswa kuwa sehemu ya safari ya maendeleo ya Wilaya ya Kalambo.
Maendeleo si jukumu la Mbunge peke yake, bali ni wajibu wa
kila mwananchi. Kama alivyowahi kusema Baba wa Taifa, Julius Kambarage Nyerere:
"Kabla hujauliza Taifa lako limekufanyia nini, jiulize
wewe umelifanyia nini Taifa lako."
Nasi tujiulize: Je, tumefanya nini kuijenga Kalambo yetu?
Kazi kuu za Mbunge ni kuwakilisha wananchi, kutetea maslahi
yao na kutunga sheria. Katika kipindi cha miezi mitano tangu achaguliwe kuwa
Mbunge wa Jimbo la Kalambo, Mhe. Edefonce Joackim Kanoni ameendelea kutekeleza
majukumu hayo kwa bidii, uwajibikaji na uzalendo.
Mara baada ya kuchaguliwa, alifanya ziara katika kata zote
23 za Jimbo la Kalambo kwa lengo la kuwashukuru wananchi na kukusanya kero
pamoja na changamoto zao ili kuziwasilisha katika mamlaka husika kwa ajili ya
utatuzi. Katika kipindi hicho cha miezi mitano, amechangia mara 18 Bungeni akiwasilisha
hoja, kero na changamoto mbalimbali zinazowakabili wananchi wa Kalambo.
Miongoni mwa masuala aliyowasilisha Serikalini ni pamoja na
umaliziaji wa magofu 143 ya vyumba vya madarasa, magofu 13 ya zahanati,
umaliziaji wa vituo vya afya vinne, ukarabati wa zahanati na vituo vya afya
chakavu, ujenzi wa vituo vya afya 15 katika kata ambazo hazina vituo vya afya,
pamoja na ujenzi wa shule za sekondari nne katika kata ambazo bado hazina shule
za sekondari.
Pia amewasilisha maombi ya kukamilisha miradi ya maji
iliyokwama baada ya kusitishwa kwa ufadhili wa Marekani, matengenezo ya
barabara zote za Halmashauri, ujenzi wa Daraja la Mto Saise lenye urefu wa mita
80, ujenzi wa kilomita 10 za barabara za lami katika Mji wa Matai, ujenzi wa
Barabara ya Mpombwe–Kipwa, upatikanaji wa fedha za kukamilisha Barabara ya
Matai–Kasesya, ujenzi wa Stendi Mpya ya Matai Ujenzi wa Kituo cha Polisi Wilaya
ya Kalambo pamoja na ukarabati wa Bandari ya Kasanga.
Kutokana na jitihada hizo, Serikali imefanikiwa kutenga
shilingi milioni 650 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya Ulumi, zimeingia
shilingi milioni 580 kwa ajili ya ujenzi wa Shule ya Sekondari Kanyezi, Zimepangwa Fedha shilingi milioni 300 kwa
ajili ya kumalizia Kituo cha Afya Mwazye, Kituo cha afya Legezamwendo, Imetengwa
shilingi milioni 138 Umaliziaji wa Kituo cha afya Kanyezi na shilingi milioni 106 kwa ajili ya Umaliziaji
wa Zahanati ya Kijiji cha Tunyi. Pia Zimepangwa milioni 60 mapato ya ndani
kwajili ya Umaliziaji kituo cha afya Samazi.
Vilevile, shilingi milioni 172 zimepatikana kwa ajili ya
kuendeleza miradi ya maji katika Kata ya Mbuluma huku zikiwa zimetengwa fedha
za kukamilisha mradi wa maji Legezamwendo.
Kwa upande wa miundombinu, shilingi milioni 300 zimepatikana
kwa ajili ya maandalizi ya ujenzi wa Stendi Mpya ya Matai. Aidha, shilingi
bilioni 1.7 tayari zimepatikana kwa ajili ya ukarabati wa barabara mbalimbali
katika Wilaya ya Kalambo na kazi zinaendelea.
Fedha za kuendeleza ujenzi wa Barabara ya Matai–Kasesya
tayari zimepatikana na mkandarasi anaendelea na utekelezaji wa kazi kwa kipande
cha kwanza kipande cha pili zimetengwa fedha. Kadhalika, fedha za ujenzi wa
barabara ya kiwango cha Nzege kutoka Rami kuelekea Bandari ya Kasanga
zilishapatikana na kazi imekamilika.
Fedha zote zilizo tengwa tunazitegemea kuingizwa baada ya
kupitishwa bajeti ya 2026-2027
Kwa upande wa Bandari ya Kasanga, fedha za ujenzi wa nguzo
za kingo za bandari zimesha patikana mkandarasi anatafutwa aweze kuanza kazi.
Aidha, Mhe. Kanoni ameendelea kujenga mahusiano mazuri na wafanyabiashara
kutoka nchi jirani ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ili kuhamasisha matumizi
ya Bandari ya Kasanga katika usafirishaji wa mizigo na biashara za kikanda.
Mhe. Kanoni pia ameendelea kutoa msukumo mkubwa katika
kukamilisha Soko la Wilaya ambalo tayari limefunguliwa na kwa sasa limekamilika
kwa zaidi ya asilimia 70. Baada ya Bajeti ya Serikali Kalambo pia inatarajia
kupata fedha za ujenzi wa kilomita tatu za barabara ya lami ndani ya Mji wa
Matai.
Katika sekta ya usafiri wa majini, ameendelea kufuatilia kwa
karibu ukamilishaji wa meli ya MV Liemba ambayo kwa sasa imefikia takribani
asilimia 65 ya ukamilishaji.
Kupitia Mfuko wa Jimbo, shilingi milioni 173 zimepatikana na
kutumika kununua bati na saruji kwa ajili ya miradi mbalimbali ya maendeleo.
Fedha hizo zimewezesha uezekaji wa masoko katika vijiji 12, umaliziaji wa
vyumba 20 vya madarasa, umaliziaji wa ofisi moja ya kijiji, ujenzi wa kivuko,
umaliziaji wa matundu saba ya vyoo pamoja na umaliziaji wa ofisi moja ya kata.
Katika upande wa utetezi wa wananchi, Mhe. Kanoni
amefanikisha wakulima wa Mambwe kupata mikopo ya kilimo yenye thamani ya zaidi
ya shilingi bilioni 3. Pia ameendelea kusaidia vijana na wanawake kupata mikopo
ya fedha bajaji, pikipiki na matrekta ili kuwainua kiuchumi.
Aidha, vijana 74 wamefanikiwa kujiunga na JKT, vijana 19
wamejiunga na mafunzo ya VETA, vijana saba wamepata ajira serikalini na zaidi
ya vijana 100 wamepata ajira za muda mfupi kupitia makampuni mbalimbali.
Amefanikiwa kununua blanketi 30 Shuka 30 folonya 60 vyenye
thamani ya shilingi milioni 1.5 kwaajili ya Kituo Cha Afya Mwimbi. Amefanikiwa
kutoa zaidi ya shilingi milioni 3 kwaajili ya kusaidia Michezo na kununua vifaa
vya michezo. Amefanikiwa kutoa zaidi ya shilingi milioni 10 kusaidia watu wenye
changamoto mbalimbali.
Mbali na hayo, amekuwa karibu na wananchi katika nyakati za
shida na furaha huku akiendelea kutetea maslahi ya makundi yote ya kijamii bila
ubaguzi.
Ndugu wananchi wa Kalambo, ndani ya miezi mitano tu ya
uongozi wake, yapo mengi yaliyofanyika na mengi zaidi yanaendelea kufuatiliwa
kwa ajili ya ustawi wa wananchi wetu. Mafanikio haya ni mwanzo wa safari ndefu
ya maendeleo inayohitaji ushirikiano wa kila mmoja wetu.
Mwenye macho haambiwi tazama. Yapo mengi yanayoonekana na
mengine yanaendelea kufuatiliwa ili kuhakikisha Kalambo inapiga hatua kubwa
zaidi za maendeleo. Tuendelee kushikamana, kumuombea afya njema Mhe. Edefonce
Joackim Kanoni, kumpa ushauri wenye kujenga na kumkosoa kwa nia njema ili aweze
kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi zaidi.
Kwa pamoja tunaweza kuijenga Kalambo yenye maendeleo na
ustawi kwa wote.
MAENDELEO KWA VITENDO
Imetolewa na:
Musa Frackison Mzopola
Katibu wa Mbunge wa Jimbo la Kalambo

