Maendeleo ya nchi na Jimbo la Kalambo si jukumu la Serikali pekee, bali ni wajibu wa kila mwananchi. Kila mmoja ana nafasi muhimu ya kuchangia maendeleo kupitia njia mbalimbali zifuatazo:
1. Kufanya kazi kwa bidii na uadilifu – Mwananchi anapofanya
kazi kwa juhudi katika kilimo, biashara, ufugaji, uvuvi au shughuli nyingine za
kiuchumi, huongeza kipato chake na kuchangia ukuaji wa uchumi wa taifa.
2. Kulipa kodi na tozo stahiki – Kodi zinazokusanywa
hutumika kujenga barabara, shule, vituo vya afya, miradi ya maji na huduma
nyingine muhimu kwa wananchi.
3. Kushiriki mikutano ya kijiji, kata na maendeleo –
Ushiriki katika vikao vya maamuzi huwapa wananchi nafasi ya kutoa maoni, kupendekeza
vipaumbele na kufuatilia utekelezaji wa miradi ya maendeleo.
4. Kutunza na kulinda miundombinu ya umma – Barabara, shule,
vituo vya afya, mabwawa na miradi mingine ni mali ya wananchi wote. Kuitunza ni
kulinda maendeleo yetu.
5. Kuhamasisha elimu na afya bora – Kuwapeleka watoto shule,
kuhimiza mahudhurio mazuri na kufuata ushauri wa wataalamu wa afya husaidia
kujenga jamii yenye maarifa na nguvu kazi bora.
6. Kudumisha amani, umoja na mshikamano – Maendeleo hayawezi
kupatikana bila amani. Wananchi wanapaswa kuepuka migogoro, chuki na vitendo
vinavyoweza kuvuruga utulivu wa jamii.
7. Kushiriki shughuli za maendeleo ya jamii – Kuchangia
nguvu kazi, mawazo au rasilimali katika miradi ya kijamii kama ujenzi wa
madarasa, zahanati na miradi ya maji ni njia muhimu ya kuharakisha maendeleo.
8. Kutoa taarifa za changamoto na kufuatilia utekelezaji
wake – Wananchi wanapaswa kutumia njia halali kufikisha kero na changamoto zao
kwa viongozi ili zipatiwe ufumbuzi kwa wakati.
Kwa ujumla, maendeleo ya Kalambo na Tanzania kwa ujumla
yatapatikana kwa haraka zaidi pale ambapo wananchi na viongozi watashirikiana,
kila mmoja akitimiza wajibu wake kwa uaminifu, uwajibikaji na uzalendo.
MAENDELEO YA KALAMBO YANAANZA NA USHIRIKI WA KILA MWANANCHI.
Imetolewa na
Musa Frackison Mzopola
Katibu wa Mbunge jimbo la Kalambo

