Ofisi ya Mbunge wa Jimbo la Kalambo, Mhe. Edefonsi Joackim Kanoni, inapenda kuwajulisha wananchi wote wa Wilaya ya Kalambo kuwa Wizara ya Mifugo na Uvuvi imekamilisha mapitio ya maombi ya mikopo yaliyowasilishwa na wananchi wa Wilaya ya Kalambo kupitia programu ya uwezeshaji wa wananchi kiuchumi.
Kutokana na mchakato huo, Wizara imetoa rasmi orodha ya wanufaika waliokidhi vigezo na kufanikiwa kupata mikopo hiyo. Wanufaika kutoka Wilaya ya Kalambo ni kama ilivyoainishwa katika orodha rasmi ya Wizara, ambayo inajumuisha:
- Rahel John Mawela – Mradi wa Mbuzi
- Faustina Cladio Msumeno – Mradi wa Kuku wa Mayai
- William Isaya Moringe – Mradi wa Mbuzi
- Mashaka Medard Jastin – Mradi wa Mfumo wa Ubaridi
- Aibini Leonard John – Mradi wa Mbuzi
- Britney Shadi Pandisha – Mradi wa Kuku wa Nyama
- Sisilia Augustino Michael – Mradi wa Mbuzi
Ofisi ya Mbunge inawapongeza wanufaika wote kwa kufanikiwa kupata fursa hiyo muhimu na inawatakia mafanikio katika utekelezaji wa miradi yao.
Aidha, wanufaika wote wanatakiwa kuhudhuria mafunzo maalumu ya ujuzi na usimamizi wa miradi yatakayofanyika kuanzia tarehe 29 Julai hadi 5 Agosti, 2026 katika ngazi ya mkoa. Mafunzo hayo yataratibiwa na Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kushirikiana na Sekretarieti za Mikoa pamoja na Mamlaka za Serikali za Mitaa.
Wanufaika wote wanasisitizwa kufika kwenye mafunzo wakiwa na kitambulisho halisi cha utambulisho kwa ajili ya uhakiki na kukamilisha taratibu zote muhimu kabla ya kupokea mikopo hiyo.
Ofisi ya Mbunge wa Jimbo la Kalambo inatoa shukrani za dhati kwa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, mawaziri, viongozi na watendaji wote wa Serikali kwa juhudi kubwa wanazoendelea kuzifanya katika kuwawezesha wananchi kiuchumi na kuwaletea maendeleo endelevu wananchi wa Wilaya ya Kalambo na Taifa kwa ujumla.
Aidha, Ofisi ya Mbunge wa Jimbo la Kalambo, kwa heshima na unyenyekevu mkubwa, inaendelea kuiomba Serikali ya Awamu ya Sita kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi kuendelea kulitafakari ombi la wavuvi wa Wilaya ya Kalambo walioomba mikopo ya vizimba vya kufugia samaki. Tunaamini Serikali yetu sikivu imekuwa mstari wa mbele katika kuwawezesha wananchi kiuchumi, hivyo tuna matumaini kuwa, kadiri rasilimali na taratibu zitakavyoruhusu, ombi hilo litapata nafasi ya kuzingatiwa. Utekelezaji wa mpango huo utachochea matumizi endelevu ya rasilimali za Ziwa Tanganyika, kuongeza uzalishaji wa samaki, kuinua kipato cha wavuvi, kufungua ajira kwa vijana na wanawake, pamoja na kuchangia ukuaji wa uchumi wa Wilaya ya Kalambo na Taifa kwa ujumla. Ofisi ya Mbunge inaendelea kuishukuru Serikali kwa juhudi kubwa inazoendelea kuzifanya katika kuwaletea wananchi maendeleo.
Mwisho, Ofisi ya Mbunge wa Jimbo la Kalambo inaendelea kuwaomba wananchi wote wa Wilaya ya Kalambo kuendelea kudumisha upendo, umoja na mshikamano, kuheshimu sheria za nchi na kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo ili kwa pamoja tuendelee kuijenga Kalambo yenye ustawi na maendeleo endelevu.
MAWASILIANO
Ofisi ya Mbunge wa Jimbo la Kalambo
Simu: 0625 850 656
Barua pepe: [email protected]
Tovuti: www.mbungekalambo.com
Imetolewa na:
Musa Frackison Mzopola
Katibu wa Mbunge wa Jimbo la Kalambo

