TAARIFA KWA UMMA
KUTOKA OFISI YA MBUNGE WA JIMBO LA KALAMBO, MHE. EDEFONSI JOACKIM KANONI
Ofisi ya Mbunge wa Jimbo la Kalambo, Mhe. Edefonsi Joackim Kanoni, inapenda kuwajulisha wananchi wote wa Jimbo la Kalambo kuwa ujenzi wa Stendi ya Kisasa, ambao unatekelezwa kwa fedha milioni 300 zilizotolewa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, tayari umeanza rasmi.
Hii ni hatua muhimu katika safari ya maendeleo ya Jimbo letu, ikiwa ni matokeo ya ushirikiano kati ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Wizara husika, viongozi wa Serikali, watendaji mbalimbali pamoja na juhudi za Mbunge wetu katika kuwasilisha na kufuatilia mahitaji ya wananchi wa Kalambo.
Kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Kalambo, tunatoa shukrani za dhati kwa Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, Mawaziri, viongozi na watendaji wote wa Serikali kwa kuendelea kusikiliza na kutekeleza mahitaji ya wananchi. Ujenzi huu ni ushahidi kuwa pale ambapo viongozi na wananchi wanashirikiana kwa dhati, maendeleo hupatikana.
Aidha, tunaendelea kuiomba Serikali kuendelea kuzipatia fedha miradi mingine ya maendeleo ambayo imewasilishwa na Mheshimiwa Mbunge kwa niaba ya wananchi pamoja na mahitaji yaliyowasilishwa na idara mbalimbali za Wilaya ya Kalambo. Tuna imani kuwa kwa ushirikiano uliopo, miradi mingi zaidi itaendelea kutekelezwa kwa manufaa ya wananchi.
Ofisi ya Mbunge inatoa wito kwa wananchi wote kuendelea kudumisha umoja, upendo, mshikamano na ushirikiano. Maendeleo si jukumu la Serikali pekee wala la Mbunge pekee, bali ni wajibu wa kila mwananchi. Tunaposhirikiana, kuheshimiana na kushiriki kikamilifu katika mipango ya maendeleo, tunaijenga Kalambo yenye ustawi na fursa kwa vizazi vya sasa na vijavyo.
Vilevile, tunawakumbusha watumishi wote wa umma kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa weledi, uadilifu na uzalendo. Wananchi wanahitaji huduma bora, za haki na zinazotolewa kwa wakati. Kila mtumishi anapaswa kutanguliza maslahi ya Taifa na wananchi mbele ya maslahi binafsi, kwani maendeleo ya nchi yetu yanategemea uwajibikaji wa kila mmoja katika nafasi yake.
Tukumbuke kuwa maendeleo ya kweli yanajengwa kwa umoja, ushirikiano, uwajibikaji na ushirikishwaji wa wananchi katika kila hatua ya maendeleo. Tukiendelea kushikamana, Kalambo itaendelea kuwa mfano wa maendeleo yanayowagusa wananchi wote.
Kazi na Utu, Tunasonga Mbele.
Imetolewa na:
Musa Frackison Mzopola
Katibu wa Mbunge
Ofisi ya Mbunge wa Jimbo la Kalambo

