KALAMBO: Kikundi cha Tuinuane kilichopo katika Kijiji cha Madibila, Jimbo la Kalambo, kimefanikiwa kunufaika na mkopo wa Shilingi Milioni 100 kwa ajili ya ununuzi wa trekta aina ya New Holland, kupitia mpango wa mikopo wa Serikali unaotekelezwa kupitia Ofisi ya Rais – Maendeleo ya Vijana.
Kikundi hicho ni miongoni mwa wanufaika wa mpango wa mikopo wenye thamani ya Shilingi Bilioni 200, unaotekelezwa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Upatikanaji wa mkopo huo umewezekana kwa juhudi za Mbunge wa Jimbo la Kalambo, Mhe. Edefonsi Joackim Kanoni, ambaye amesaidia kufuatilia na kuwezesha upatikanaji wa fursa hiyo kupitia Ofisi ya Rais – Maendeleo ya Vijana.
Trekta aina ya New Holland, ambayo ni miongoni mwa matrekta bora na imara, inatarajiwa kuongeza tija katika shughuli za kilimo, kupunguza changamoto za upatikanaji wa huduma za kilimo na kuchochea maendeleo ya kiuchumi kwa wanakikundi pamoja na wananchi wa Kalambo kwa ujumla.
Ofisi ya Mbunge wa Jimbo la Kalambo imetoa shukrani za dhati kwa Serikali ya Awamu ya Sita, chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kujali, kuthamini na kuunga mkono juhudi za maendeleo ya wananchi wa Kalambo.
Aidha, Ofisi ya Mbunge imetoa shukrani maalum kwa Mhe. Joel Arthur Nanauka, Waziri wa Ofisi ya Rais – Maendeleo ya Vijana, pamoja na Mawaziri na watendaji wote wa Serikali, kwa juhudi na ushirikiano wao katika kuhakikisha wananchi wanapata fursa za kiuchumi na mikopo yenye tija.
Pamoja na mafanikio hayo, Ofisi ya Mbunge inaendelea kuiomba Serikali kuendelea kutoa na kuongeza fursa za mikopo kwa wananchi wa Kalambo, hususan mikopo ya vizimba katika Ziwa Tanganyika pamoja na mikopo ya ufugaji, ili kuwawezesha wananchi wengi zaidi kushiriki katika shughuli za uzalishaji na kujikwamua kiuchumi.
Ofisi ya Mbunge inatoa wito kwa wananchi wote wa Kalambo kuendelea kudumisha upendo, umoja na mshikamano, kwa kuwa umoja na mshikamano wa wananchi ni msingi muhimu katika kuendeleza na kuijenga Kalambo yenye maendeleo endelevu.
Imetolewa na:
MUSA FRACKISON MZOPOLA
KATIBU WA MBUNGE
JIMBO LA KALAMBO

