📰 HABARI MPYA
Inapakia habari...

MIKOPO YA HALMASHAURI SIYO BAHATI – NI FURSA INAYOHITAJI MAANDALIZI: ELEWA KWANZA, KISHA FANIKIWA

MIKOPO YA HALMASHAURI SIYO BAHATI – NI FURSA INAYOHITAJI MAANDALIZI: ELEWA KWANZA, KISHA FANIKIWA

 

Wananchi wenzangu wa Jimbo la Kalambo,

Kumekuwa na maswali mengi kuhusu mikopo inayotolewa na Serikali na Halmashauri. Wapo wanaoamini kuwa mikopo haitoki, wengine hudhani masharti ni magumu, na wengine huanzisha vikundi kwa lengo la kusubiri fedha za mkopo pekee. Ukweli ni kwamba, mafanikio ya kupata mkopo huanza na kuwa na uelewa sahihi wa mfumo wa utoaji wake.

Aina za mikopo inayotolewa na Serikali

Kwa ujumla, kuna aina kuu tatu za mikopo inayowezesha wananchi kujikwamua kiuchumi.

1. Mikopo ya Wizara

Hii imegawanyika katika makundi mawili:

  • Mikopo isiyo na riba inayotolewa kupitia Wizara inayosimamia maendeleo ya jamii.
  • Mikopo yenye riba ya asilimia 5 inayotolewa kupitia wizara mbalimbali za kisekta kwa ajili ya shughuli maalumu za kiuchumi.

2. Mikopo ya Wajasiriamali Wadogo

Hii hutolewa kupitia taasisi za benki kwa wajasiriamali wadogo na kwa kawaida huwa na riba ya takribani asilimia 7 kulingana na utaratibu wa mpango husika.

3. Mikopo ya Halmashauri (Asilimia 10)

Hii ni mikopo isiyo na riba, na ndiyo ambayo wananchi wengi huizungumza. Hata hivyo, ipo haja ya kuifahamu kwa undani ili kuondoa dhana potofu zilizojengeka.

Ukweli kuhusu Mikopo ya Halmashauri

Jambo la kwanza ambalo kila mwananchi anatakiwa kulielewa ni kwamba, hakuna fedha zinazokuwa zimekaa pembeni zikisubiri wakopaji.

Fedha za mikopo ya Halmashauri hutokana na asilimia 10 ya mapato ya ndani yanayokusanywa na Halmashauri. Kadiri mapato yanavyoongezeka, ndivyo kiwango cha fedha za mikopo kinavyoongezeka pia.

Hivyo, kiasi cha fedha kinachotolewa hutegemea mapato halisi yaliyopatikana katika kipindi husika.

Utaratibu wa utoaji wa mikopo

Kwa kawaida, kila baada ya miezi mitatu Halmashauri hufungua dirisha la maombi ya mikopo.

Utaratibu huwa kama ifuatavyo:

  • Halmashauri hutoa tangazo rasmi la mikopo na kutangaza kiasi cha fedha kilichopo kwa ajili ya kukopesha.
  • Wananchi hupewa takribani mwezi mmoja kuwasilisha maombi.
  • Baada ya muda wa maombi kuisha, Halmashauri hutumia mwezi mmoja kukagua vikundi na miradi yao.
  • Siku 15 hutumika kutembelea na kuhakiki miradi.
  • Siku 15 zinazofuata hutumika kuidhinisha na kutoa mikopo kwa vikundi vilivyokidhi vigezo.

Nani anastahili kuomba?

Mikopo hii hutolewa kwa:

  • Vikundi vya Vijana.
  • Vikundi vya Wanawake.
  • Vikundi vya Watu wenye Ulemavu.

Ili kikundi kipate mkopo lazima:

  • Kiwe kimesajiliwa kwa mujibu wa sheria.
  • Kiwe na mradi unaoendelea na unaoonekana kufanya kazi.
  • Kiwasilishe barua ya maombi.
  • Kiambatishe mpango wa matumizi ya fedha na namna zitakavyokuza mradi.
  • Kiambatishe muhtasari wa kikao unaoonyesha wanakikundi wamekubaliana kuomba mkopo.

Kwa nini baadhi ya vikundi havipati mkopo?

Zipo sababu kuu mbili:

Kwanza, kikundi kutokukidhi vigezo vilivyowekwa.

Pili, fedha zilizopo zinaweza kuwa ndogo kuliko mahitaji ya waombaji.

Kwa mfano, kama Halmashauri ina shilingi milioni 100 za kukopesha lakini maombi yote yanafikia milioni 300, ni wazi kuwa si kila kikundi kitapata mkopo katika awamu hiyo. Vikundi vitakavyokosa si kwamba havistahili, bali vitasubiri dirisha litakalofuata kulingana na fedha zitakazopatikana.

Changamoto kubwa iliyopo

Wananchi wengi bado hawajapata elimu ya kutosha kuhusu mfumo huu wa mikopo.

Wengi huanzisha vikundi kwa lengo la kupata mkopo pekee, badala ya kuanza kujenga shughuli za kiuchumi kwa nguvu zao. Wanapofika hatua ya ukaguzi hukosa sifa kwa sababu hawana mradi unaoendelea. Baada ya kukosa mkopo, vikundi huvunjika na kuanza kusema kuwa masharti ni magumu au fedha hazitoki.

Huo si ukweli.

Mkopo unalenga kuimarisha biashara au mradi uliopo, si kuanzisha ndoto ambayo bado haijaanza kutekelezwa.

Wito kwa Wanakalambo

Ndugu zangu Wanakalambo, ni wakati wa kubadili mtazamo.

Tusiunde vikundi kwa ajili ya kusubiri mkopo pekee. Tuanzishe miradi, tushirikiane, tutoe mchango wetu na tujenge msingi imara wa kujitegemea. Kikundi kinachoonyesha uwezo wa kufanya kazi kina nafasi kubwa zaidi ya kupata mkopo na hata kuurejesha kwa mafanikio.

Tusisubiri fedha zitubadilishe maisha; tuanze sisi kubadili maisha yetu, kisha fedha zitakuwa nyenzo ya kutuongezea nguvu.

Kumbukeni, hakuna mafanikio bila juhudi.

Anza leo. Amini unaweza. Ondoa fikra za kusema "siwezi" na ujenge imani ya kusema "naweza." Mtazamo huo ndiyo hatua ya kwanza kuelekea mafanikio ya kiuchumi kwa mtu binafsi, kikundi na jamii kwa ujumla.

Imetolewa na:

Musa Frackison Mzopola
Katibu wa Mbunge, Jimbo la Kalambo


MATUKIO KWA NJIA YA PICHA

Inapakia picha...

HABARI MAARUFU

ZIARA YA MHE. KANONI KATIKA JIMBO LA KALAMBO IMEAIRISHWA; HIKI NDICHO KILICHOSABABISHA.

  Ofisi ya Mbunge wa Jimbo la Kalambo, Mhe. Edefonsi Joackim Kanoni , inapenda kuwataarifu wananchi wote wa Jimbo la Kalambo na umma kwa ujumla kuwa ziara iliyokuwa imepangwa kufanyika kuanzia tarehe 20 Julai 2026 hadi tarehe 10 Agosti 2026 imeahirishwa. Uamuzi huo umetokana na zuio la Serikali kuhusu kufanyika kwa mikutano ya hadhara katika kipindi hiki. Ofisi ya Mbunge inaomba radhi kwa usumbufu uliojitokeza na inaendelea kuwashukuru wananchi kwa ushirikiano na uelewa wao. Kwa taarifa zaidi na maendeleo ya shughuli za Ofisi ya Mbunge wa Jimbo la Kalambo, tembelea: www.mbungekalambo.com Imetolewa na: Musa Frackison Mzopola Katibu wa Mbunge, Jimbo la Kalambo

HATIMAYE! ORODHA RASMI YA WANUFAIKA WA MIKOPO YA WIZARA YA MIFUGO NA UVUVI KWA WILAYA YA KALAMBO YATOLEWA – WANUFAIKA WOTE WATAKIWA KUHUDHURIA MAFUNZO MUHIMU

  TAARIFA KWA UMMA Ofisi ya Mbunge wa Jimbo la Kalambo, Mhe. Edefonsi Joackim Kanoni , inapenda kuwajulisha wananchi wote wa Wilaya ya Kalambo kuwa Wizara ya Mifugo na Uvuvi imekamilisha mapitio ya maombi ya mikopo yaliyowasilishwa na wananchi wa Wilaya ya Kalambo kupitia programu ya uwezeshaji wa wananchi kiuchumi. Kutokana na mchakato huo, Wizara imetoa rasmi orodha ya wanufaika waliokidhi vigezo na kufanikiwa kupata mikopo hiyo. Wanufaika kutoka Wilaya ya Kalambo ni kama ilivyoainishwa katika orodha rasmi ya Wizara, ambayo inajumuisha: Rahel John Mawela – Mradi wa Mbuzi Faustina Cladio Msumeno – Mradi wa Kuku wa Mayai William Isaya Moringe – Mradi wa Mbuzi Mashaka Medard Jastin – Mradi wa Mfumo wa Ubaridi Aibini Leonard John – Mradi wa Mbuzi Britney Shadi Pandisha – Mradi wa Kuku wa Nyama Sisilia Augustino Michael – Mradi wa Mbuzi Ofisi ya Mbunge inawapongeza wanufaika wote kwa kufanikiwa kupata fursa hiyo muhimu na inawatakia mafanikio katika utekelezaji wa ...

ZIARA YA MIKUTANO YA HADHARA YA MHE. EDEFONSI JOACKIM KANONI MBUNGE JIMBO LA KALAMBO YATANGAZWA

  Ofisi ya Mbunge wa Jimbo la Kalambo inapenda kuwataarifu wananchi wote wa Jimbo la Kalambo kuwa Mhe. Edefonsi Joackim Kanoni (Mb), Mbunge wa Jimbo la Kalambo, atafanya ziara ya mikutano ya hadhara katika kata na vijiji mbalimbali vya jimbo kuanzia tarehe 20 Julai, 2026 hadi tarehe 10 Agosti, 2026, kwa mujibu wa ratiba iliyoambatanishwa.    Ziara hii inalenga kuimarisha mawasiliano kati ya Mbunge na wananchi kwa kukutana nao ana kwa ana, kusikiliza maoni, kero na changamoto zinazowakabili, pamoja na kupokea mapendekezo yatakayosaidia kuboresha huduma za kijamii na kuharakisha maendeleo ya Jimbo la Kalambo. Aidha, Mhe. Mbunge atatoa mrejesho kuhusu utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kueleza mipango ya maendeleo inayotarajiwa kutekelezwa katika maeneo mbalimbali ya jimbo. Wananchi watapata fursa ya kuuliza maswali, kutoa maoni yao na kushiriki katika kujadili masuala muhimu yanayohusu maendeleo ya kata na vijiji vyao. Ushiriki wa wananchi katika mikutano hii ni msingi m...