Wananchi wenzangu wa Jimbo la Kalambo,
Kumekuwa na maswali mengi kuhusu mikopo inayotolewa na Serikali na Halmashauri. Wapo wanaoamini kuwa mikopo haitoki, wengine hudhani masharti ni magumu, na wengine huanzisha vikundi kwa lengo la kusubiri fedha za mkopo pekee. Ukweli ni kwamba, mafanikio ya kupata mkopo huanza na kuwa na uelewa sahihi wa mfumo wa utoaji wake.
Aina za mikopo inayotolewa na Serikali
Kwa ujumla, kuna aina kuu tatu za mikopo inayowezesha wananchi kujikwamua kiuchumi.
1. Mikopo ya Wizara
Hii imegawanyika katika makundi mawili:
- Mikopo isiyo na riba inayotolewa kupitia Wizara inayosimamia maendeleo ya jamii.
- Mikopo yenye riba ya asilimia 5 inayotolewa kupitia wizara mbalimbali za kisekta kwa ajili ya shughuli maalumu za kiuchumi.
2. Mikopo ya Wajasiriamali Wadogo
Hii hutolewa kupitia taasisi za benki kwa wajasiriamali wadogo na kwa kawaida huwa na riba ya takribani asilimia 7 kulingana na utaratibu wa mpango husika.
3. Mikopo ya Halmashauri (Asilimia 10)
Hii ni mikopo isiyo na riba, na ndiyo ambayo wananchi wengi huizungumza. Hata hivyo, ipo haja ya kuifahamu kwa undani ili kuondoa dhana potofu zilizojengeka.
Ukweli kuhusu Mikopo ya Halmashauri
Jambo la kwanza ambalo kila mwananchi anatakiwa kulielewa ni kwamba, hakuna fedha zinazokuwa zimekaa pembeni zikisubiri wakopaji.
Fedha za mikopo ya Halmashauri hutokana na asilimia 10 ya mapato ya ndani yanayokusanywa na Halmashauri. Kadiri mapato yanavyoongezeka, ndivyo kiwango cha fedha za mikopo kinavyoongezeka pia.
Hivyo, kiasi cha fedha kinachotolewa hutegemea mapato halisi yaliyopatikana katika kipindi husika.
Utaratibu wa utoaji wa mikopo
Kwa kawaida, kila baada ya miezi mitatu Halmashauri hufungua dirisha la maombi ya mikopo.
Utaratibu huwa kama ifuatavyo:
- Halmashauri hutoa tangazo rasmi la mikopo na kutangaza kiasi cha fedha kilichopo kwa ajili ya kukopesha.
- Wananchi hupewa takribani mwezi mmoja kuwasilisha maombi.
- Baada ya muda wa maombi kuisha, Halmashauri hutumia mwezi mmoja kukagua vikundi na miradi yao.
- Siku 15 hutumika kutembelea na kuhakiki miradi.
- Siku 15 zinazofuata hutumika kuidhinisha na kutoa mikopo kwa vikundi vilivyokidhi vigezo.
Nani anastahili kuomba?
Mikopo hii hutolewa kwa:
- Vikundi vya Vijana.
- Vikundi vya Wanawake.
- Vikundi vya Watu wenye Ulemavu.
Ili kikundi kipate mkopo lazima:
- Kiwe kimesajiliwa kwa mujibu wa sheria.
- Kiwe na mradi unaoendelea na unaoonekana kufanya kazi.
- Kiwasilishe barua ya maombi.
- Kiambatishe mpango wa matumizi ya fedha na namna zitakavyokuza mradi.
- Kiambatishe muhtasari wa kikao unaoonyesha wanakikundi wamekubaliana kuomba mkopo.
Kwa nini baadhi ya vikundi havipati mkopo?
Zipo sababu kuu mbili:
Kwanza, kikundi kutokukidhi vigezo vilivyowekwa.
Pili, fedha zilizopo zinaweza kuwa ndogo kuliko mahitaji ya waombaji.
Kwa mfano, kama Halmashauri ina shilingi milioni 100 za kukopesha lakini maombi yote yanafikia milioni 300, ni wazi kuwa si kila kikundi kitapata mkopo katika awamu hiyo. Vikundi vitakavyokosa si kwamba havistahili, bali vitasubiri dirisha litakalofuata kulingana na fedha zitakazopatikana.
Changamoto kubwa iliyopo
Wananchi wengi bado hawajapata elimu ya kutosha kuhusu mfumo huu wa mikopo.
Wengi huanzisha vikundi kwa lengo la kupata mkopo pekee, badala ya kuanza kujenga shughuli za kiuchumi kwa nguvu zao. Wanapofika hatua ya ukaguzi hukosa sifa kwa sababu hawana mradi unaoendelea. Baada ya kukosa mkopo, vikundi huvunjika na kuanza kusema kuwa masharti ni magumu au fedha hazitoki.
Huo si ukweli.
Mkopo unalenga kuimarisha biashara au mradi uliopo, si kuanzisha ndoto ambayo bado haijaanza kutekelezwa.
Wito kwa Wanakalambo
Ndugu zangu Wanakalambo, ni wakati wa kubadili mtazamo.
Tusiunde vikundi kwa ajili ya kusubiri mkopo pekee. Tuanzishe miradi, tushirikiane, tutoe mchango wetu na tujenge msingi imara wa kujitegemea. Kikundi kinachoonyesha uwezo wa kufanya kazi kina nafasi kubwa zaidi ya kupata mkopo na hata kuurejesha kwa mafanikio.
Tusisubiri fedha zitubadilishe maisha; tuanze sisi kubadili maisha yetu, kisha fedha zitakuwa nyenzo ya kutuongezea nguvu.
Kumbukeni, hakuna mafanikio bila juhudi.
Anza leo. Amini unaweza. Ondoa fikra za kusema "siwezi" na ujenge imani ya kusema "naweza." Mtazamo huo ndiyo hatua ya kwanza kuelekea mafanikio ya kiuchumi kwa mtu binafsi, kikundi na jamii kwa ujumla.
Imetolewa na:
Musa Frackison Mzopola
Katibu wa Mbunge, Jimbo la Kalambo

