Ofisi ya Mbunge wa Jimbo la Kalambo, Mhe. Edefonsi Joackim Kanoni, inapenda kutoa shukrani za dhati kwa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, pamoja na Mawaziri, viongozi na watendaji wote wa Serikali kwa kuendelea kusikiliza na kutekeleza kwa vitendo maombi yaliyowasilishwa kwa ajili ya maendeleo ya wananchi wa Jimbo la Kalambo.
Ofisi ya Mbunge imepokea kwa furaha taarifa ya kutolewa kwa fedha za utekelezaji wa miradi mbalimbali ya elimu, ikiwa ni pamoja na ujenzi wa madarasa matano (5) na matundu kumi (10) ya vyoo katika Shule ya Msingi Msoma, Kata ya Mwazye, ujenzi wa madarasa matano (5) na matundu kumi (10) ya vyoo katika Shule ya Msingi Mzungwa, Kata ya Mambwenkoswe, pamoja na fedha za ujenzi wa Kituo cha Walimu katika Kijiji cha Kalembe, Kata ya Mambwenkoswe
Hatua hii ni uthibitisho kuwa Serikali inaendelea kuwajali na kuwathamini wananchi wa Kalambo kwa kutekeleza miradi yenye lengo la kuboresha huduma za elimu na kuinua ustawi wa jamii.
Pamoja na mafanikio hayo, Ofisi ya Mbunge inaendelea kuiomba Serikali kuidhinisha fedha zaidi kwa ajili ya kukamilisha miradi mingine ya maendeleo ambayo imewasilishwa, ili wananchi wa Kalambo waendelee kunufaika na huduma bora katika sekta mbalimbali.
Aidha, Mhe. Kanoni anatoa wito kwa wananchi wote wa Jimbo la Kalambo kuendelea kudumisha umoja, upendo, mshikamano na ushirikiano, kwani maendeleo ya kweli yanapatikana pale wananchi wanaposhirikiana na kuunga mkono juhudi za Serikali katika kutekeleza miradi ya maendeleo.
Ofisi ya Mbunge wa Jimbo la Kalambo inaendelea kuwahakikishia wananchi kuwa itaendelea kusimamia na kufuatilia kwa karibu utekelezaji wa ahadi na miradi yote ya maendeleo kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.
Imetolewa na
Musa Frackison Mzopola
Katibu wa Mbunge Jimbo la Kalambo

