Kalambo, Rukwa | Julai 29, 2026
Ofisi ya Mbunge wa Jimbo la Kalambo, Mhe. Edefonsi Joachim Kanoni, inapenda kuwajulisha wananchi wa Wilaya ya Kalambo kuwa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan imekabidhi rasmi gari jipya la wagonjwa kwa ajili ya kuhudumia wananchi wa Ukanda wa Mambwe.
Makabidhiano hayo yalifanyika tarehe 29 Julai, 2026 katika Kata ya Legezamwendo, yakiongozwa na Mhe. Charles Makongoro Nyerere, Mkuu wa Mkoa wa Rukwa. Gari hilo linatarajiwa kuboresha huduma za dharura na kupunguza changamoto za usafirishaji wa wagonjwa katika Ukanda wa Mambwe.
Akizungumza wakati wa hafla ya makabidhiano, Mhe. Charles Makongoro Nyerere aliwataka wananchi kulitunza gari hilo ili liweze kutoa huduma kwa muda mrefu. Aidha, aliwahimiza wananchi kumshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuwajali wananchi wa Kalambo kupitia maboresho makubwa ya huduma za afya.
Kwa upande wa Wilaya ya Kalambo, Mkuu wa Mkoa aliwataka wananchi kumpongeza Mbunge wa Jimbo la Kalambo, Mhe. Edefonsi Joachim Kanoni, kwa juhudi zake za kuomba na kufuatilia kwa karibu upatikanaji wa gari hilo hadi kufanikisha kupatikana kwake.
Mhe. Charles Makongoro Nyerere alisema kuwa wakati Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, Prof. Riziki Silas Shemdoe, alipofanya ziara mkoani Rukwa siku 14 zilizopita, alieleza kuwa Mbunge Kanoni ni mmoja wa wabunge wanaofuatilia kwa karibu mahitaji ya wananchi wao na hakuchoka kuwasilisha maombi serikalini, jambo lililochangia kupatikana kwa gari hilo.
Aidha, Mkuu wa Mkoa alisisitiza kuwa viongozi wanapaswa kuwa na utamaduni wa kufuatilia maendeleo ya wananchi badala ya kusubiri kila jambo lifike kwa utaratibu wa kawaida. Alibainisha kuwa kati ya magari 20 ya wagonjwa yaliyotolewa kwa Tanzania Bara, Mkoa wa Rukwa umefanikiwa kupata magari mawili kutokana na juhudi hizo.
Aliwahimiza pia wananchi kuendelea kushirikiana na Serikali kwa kujenga nyumba za watumishi wa afya ili kuwavutia na kuwawezesha kutoa huduma katika mazingira bora.
Kwa upande wake, Mbunge wa Jimbo la Kalambo, Mhe. Edefonsi Joachim Kanoni, alimshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuijali Kalambo kupitia uwekezaji mkubwa katika sekta ya afya. Vilevile alimshukuru Prof. Riziki Silas Shemdoe, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, pamoja na mawaziri, manaibu mawaziri na watendaji wote wa Serikali kwa ushirikiano walioutoa hadi kufanikisha upatikanaji wa gari hilo.
Mbunge Kanoni aliwahimiza wananchi kulitunza gari hilo ili kiendelee kuwahudumia kwa muda mrefu. Aidha, aliishukuru Serikali ya Awamu ya Sita kwa kuendelea kuimarisha huduma za afya Wilayani Kalambo kupitia utoaji wa shilingi milioni 438 kwa ajili ya ukamilishaji wa Vituo vya Afya vya Legezamwendo, Mwazye na Samazi, pamoja na shilingi milioni 138 kwa ajili ya ukamilishaji wa Kituo cha Afya cha Kanyezi.
Mbunge huyo aliwaomba wananchi kuendelea kutoa ushirikiano kwa Serikali ya Awamu ya Sita kwa kuwa imeendelea kuwajali na kuwathamini. Pia aliwasihi kuendeleza umoja, mshikamano na upendo ili kuharakisha maendeleo ya Wilaya ya Kalambo.
Kwa upande wao, wananchi wa Ukanda wa Mambwe walimshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, Mbunge Mhe. Edefonsi Joachim Kanoni, pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, Mhe. Charles Makongoro Nyerere, kwa kufanikisha upatikanaji wa gari hilo. Kama ishara ya shukrani na kuthamini juhudi hizo, wananchi walimkabidhi Mkuu wa Mkoa mbuzi.
KAZI NA UTU, TUNASONGA MBELE
Imetolewa na:
Musa Frackison Mzopola
Katibu wa Mbunge, Jimbo la Kalambo











