Mhe. Edefonsi Joackim Kanoni, Mbunge wa Jimbo la Kalambo, amewatakia Wanakalambo na Watanzania wote, hususan Waislamu, Maulidi njema yenye furaha, upendo, mshikamano na amani.
Katika salamu zake za Maulidi, Mhe. Kanoni amesema sikukuu kama hii ni wakati muhimu wa kutafakari na kujikumbusha kumrudia Muumba wetu, kuishi kwa kufuata mafundisho mema, kutenda mema, kusaidiana na kuwa na upendo na huruma kwa wengine.
Amesema Maulidi inapaswa kuwa zaidi ya sherehe, bali iwe fursa ya kujenga jamii yenye maadili mema, upendo, umoja, mshikamano na amani, kwa kuwa mambo hayo ndiyo msingi wa maendeleo ya familia, jamii na taifa kwa ujumla.
Mhe. Kanoni amesisitiza umuhimu wa amani ya Tanzania, akieleza kuwa amani ni tunu kubwa ambayo kila Mtanzania anapaswa kuilinda na kuithamini.
Amesema iwapo amani itapotea, shughuli nyingi za kijamii, kiuchumi na hata za ibada zinaweza kusimama, jambo ambalo linaweza kuathiri uchumi na maendeleo ya nchi.
Katika maadhimisho haya ya Maulidi, Mhe. Kanoni amewaomba Watanzania kuwaombea viongozi wa nchi, ili waendelee kuiongoza Tanzania kwa hekima, upendo, mshikamano na kulinda amani ya taifa.
Ametoa wito kwa wananchi kuwaombea Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, pamoja na Mawaziri, Naibu Mawaziri, Wabunge na viongozi wengine wa Serikali, ili Mungu awape hekima, afya na uwezo wa kulitumikia taifa kwa uadilifu na kuhakikisha amani na mshikamano vinaendelea kudumu.
Aidha, amewaomba Watanzania kuwaombea Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na watendaji wote wa Serikali, ili katika majukumu yao waweze kulitumikia taifa kwa weledi, uadilifu na kwa kuzingatia maslahi ya Watanzania.
Mhe. Kanoni amewataka Wanakalambo na Watanzania wote kutumia siku hii ya Maulidi kuimarisha udugu, kuvumiliana, kusaidiana na kuendeleza utamaduni wa kuishi pamoja kwa amani bila kujali tofauti za dini, itikadi au makundi.
Amesema Tanzania ni yetu sote, hivyo kila mmoja ana wajibu wa kuilinda amani, umoja na mshikamano ambao taifa limejenga kwa miaka mingi.
“Amani ndiyo tunu yetu. Tuilinde, tuiombee na tuiendeleze kwa vitendo, kwa sababu bila amani hakuna maendeleo endelevu.”
Mhe. Edefonsi Joackim Kanoni amewatakia Wanakalambo, Watanzania wote na Waislamu kote nchini Maulidi yenye baraka, akiwataka kutumia siku hiyo kutenda mema, kueneza upendo na kuendelea kumuomba Mwenyezi Mungu ailinde Tanzania na watu wake.
Maulidi Njema!
Amani, Upendo na Mshikamano kwa Taifa Letu.
Imetolewa na:
Musa Frackison Mzopola
Katibu wa Mbunge Jimbo la Kalambo


💬 Toa Maoni Kuhusu Habari Hii
Umemaliza kusoma habari hii? Tupe maoni, mtazamo au swali lako hapa chini.
Comments
Post a Comment