Ofisi ya Mbunge wa Jimbo la Kalambo, Mhe. Edefonsi Joackim Kanoni, imepokea kwa masikitiko makubwa taarifa ya kifo cha kijana Baracka Leonard Msili, mkazi wa Santamaria, Wilaya ya Kalambo, Mkoa wa Rukwa, kilichotokea katika eneo hilo.
Katika kipindi hiki kigumu cha majonzi, Mhe. Edefonsi Joackim Kanoni anatoa pole za dhati kwa ndugu, jamaa, marafiki na wote walioguswa na msiba huu mkubwa.
Tunatambua kuwa kumpoteza kijana katika umri mdogo ni pigo kubwa kwa familia, ndugu na jamii kwa ujumla. Tunawaombea Mwenyezi Mungu awape nguvu, faraja na uvumilivu katika kipindi hiki cha majonzi, na ailaze roho ya marehemu mahali pema peponi.
Kifo kinatukumbusha kuwa maisha ya mwanadamu ni mafupi na hakuna anayejua siku wala saa yake. Hivyo, kila mmoja wetu anapaswa kuishi kwa kufanya mema, kujenga mahusiano mazuri na jamii, kusaidia wengine na kuweka alama njema katika maisha yake ili atakapoondoka duniani akumbukwe kwa mazuri aliyoyafanya.
Aidha, Ofisi ya Mbunge inatoa rai kwa madereva wote wa pikipiki na magari kuzingatia sheria na kanuni za usalama barabarani, kuwa makini wakati wote wanapokuwa barabarani na kuepuka vitendo vinavyoweza kusababisha ajali na kupoteza maisha.
Pia tunatoa wito kwa maafisa usalama barabarani kuendelea kusimamia sheria kwa ufanisi na kutoa elimu kwa watumiaji wa barabara, hususan vijana wanaotumia pikipiki, ili kusaidia kupunguza ajali na kulinda maisha ya wananchi.
Maisha ya kila mmoja yana thamani kubwa, hivyo ni jukumu letu sote kuhakikisha tunalinda maisha kwa kuchukua tahadhari na kuzingatia usalama katika kila hatua.
Imetolewa na:
Musa Frackison Mzopola
Katibu wa Mbunge Jimbo la Kalambo


💬 Toa Maoni Kuhusu Habari Hii
Umemaliza kusoma habari hii? Tupe maoni, mtazamo au swali lako hapa chini.
Comments
Post a Comment