Ofisi ya Mbunge Jimbo la Kalambo inapenda kuwataarifu wananchi wote wa Jimbo la Kalambo kuwa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuonesha dhamira ya dhati ya kuboresha huduma za afya kwa kutenga zaidi ya shilingi bilioni 1.2 kwa ajili ya ujenzi na ukamilishaji wa vituo vya afya na zahanati mbalimbali ndani ya Jimbo la Kalambo.
Akizungumza wakati wa kukabidhi gari la wagonjwa (Ambulance) katika Kata ya Legezamwendo, Mbunge wa Jimbo la Kalambo, Mhe. Edefonsi Joackim Kanoni, amesema kuwa uwekezaji huo unaonesha wazi jinsi Serikali inavyoweka kipaumbele katika kuimarisha sekta ya afya kwa kusogeza huduma karibu na wananchi ili kuhakikisha kila mwananchi anapata huduma bora, salama na kwa wakati. Amesema dhamira ya Serikali ni kuendelea kuboresha afya za wananchi, kupunguza vifo vinavyoweza kuzuilika, kuimarisha huduma za afya ya mama na mtoto, pamoja na kuongeza ustawi wa jamii kupitia huduma bora za matibabu.
Mhe. Kanoni amesema kuwa katika utekelezaji wa mpango huo, Serikali imetenga shilingi milioni 650 kupitia Serikali Kuu kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya Ulumi, shilingi milioni 300 kwa ajili ya umaliziaji wa Vituo vya Afya Mwazye na Legezamwendo, shilingi milioni 60 kutoka mapato ya Halmashauri kwa ajili ya umaliziaji wa Kituo cha Afya Samazi, shilingi milioni 138 kwa ajili ya umaliziaji wa Kituo cha Afya Kanyezi, pamoja na shilingi milioni 106 kwa ajili ya umaliziaji wa Zahanati ya Kijiji cha Tunyi, Kata ya Mambwenkoswe.
Amesema kukamilika kwa miradi hiyo kutapunguza adha ya wananchi kusafiri umbali mrefu kutafuta huduma za matibabu, kuboresha huduma za afya ya mama na mtoto, kuongeza uwezo wa kuhudumia wagonjwa wa dharura, kuimarisha mazingira ya kazi kwa watumishi wa afya na kuongeza upatikanaji wa huduma bora za afya kwa wananchi wote. Aidha, amesema uwekezaji huo utachochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi kwa kuwa wananchi wenye afya njema hushiriki kikamilifu katika shughuli za uzalishaji na maendeleo ya Taifa.
Mbunge huyo ameishukuru kwa dhati Serikali ya Awamu ya Sita kwa kuendelea kupeleka fedha za maendeleo katika Jimbo la Kalambo. Pia ametoa shukrani kwa Mawaziri, Manaibu Mawaziri, viongozi wa Mkoa wa Rukwa, Wilaya ya Kalambo pamoja na watendaji wote wa Serikali kwa ushirikiano mkubwa wanaouonesha katika kuhakikisha miradi ya maendeleo inatekelezwa na kuwanufaisha wananchi.
Aidha, Mhe. Kanoni amewaomba wananchi wa Jimbo la Kalambo kuendelea kusimamia kwa karibu utekelezaji wa miradi hiyo ili fedha zilizotengwa zitumike kwa uadilifu, uwazi na ufanisi. Amesisitiza kuwa fedha hizo ni mali ya wananchi zinazotokana na kodi zao, hivyo kila mwananchi ana wajibu wa kuzilinda na kuhakikisha miradi inakamilika kwa viwango vinavyokusudiwa.
Katika hitimisho la hotuba yake, Mhe. Kanoni ametoa wito kwa wananchi kuendelea kudumisha upendo, amani, umoja na mshikamano, akieleza kuwa misingi hiyo ndiyo nguzo muhimu ya maendeleo endelevu. Amesema kwa kuendelea kushirikiana na kuiunga mkono Serikali katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo, Jimbo la Kalambo litaendelea kupiga hatua kubwa za maendeleo.
KAZI NA UTU, TUNASONGA MBELE.
Imetolewa na:
Musa Frackison Mzopola
Katibu wa Mbunge Jimbo la Kalambo

