Mbunge wa Jimbo la Kalambo, Mhe. Edifonsi Joackim Kanoni, ameteuliwa rasmi kuwa mmoja wa wajumbe 10 wanaounda Chama cha Kirafiki cha Kibunge kati ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Bunge la India.
Kwa mujibu wa barua ya Katibu wa Bunge yenye kumbukumbu
namba QA.203/261/01/48 ya tarehe 15 Juni 2026, uteuzi huo umefanywa na Spika wa
Bunge, Mhe. Mussa Azzan Zungu (Mb), kwa lengo la kuimarisha ushirikiano,
urafiki na diplomasia ya kibunge kati ya Tanzania na India.
Chama hicho kinaundwa na wabunge 10 walioteuliwa kutoka
Bunge la Tanzania kwa ajili ya kushiriki shughuli mbalimbali za kuendeleza
mahusiano ya kirafiki na kubadilishana uzoefu katika sekta mbalimbali za
maendeleo kati ya nchi hizo mbili.
Aidha, Balozi wa India nchini Tanzania anatarajiwa kukutana
na kufanya mazungumzo na wajumbe wa chama hicho tarehe 24 au 25 Juni 2026
katika Ofisi za Bunge jijini Dodoma, ikiwa ni sehemu ya kuimarisha ushirikiano
kati ya mabunge ya nchi hizo mbili.
Uteuzi wa Mhe. Kanoni ni heshima kubwa kwa Jimbo la Kalambo,
Mkoa wa Rukwa na Taifa kwa ujumla, ukiwa ni ishara ya imani kubwa aliyopewa
katika kuwakilisha Tanzania kwenye masuala ya ushirikiano wa kimataifa kupitia
diplomasia ya kibunge.
Imetolewa
Musa Frackison Mzopola
Katibu wa Mbunge jimbo la Kalambo

